Wednesday, March 23, 2016

Wkb

Mshukiwa aliyekuwa akisakwa sana kuhusiana na mashambulio ya Brussels amekamatwa na maafisa wa usalama, vyombo vya habari Ubelgiji vimeripoti. Baadhi ya vyombo vya habari limetaja jina lake kuwa Najim Laachraoui. Wadadisi wanasema Laachraoui anaaminika kuwa mtaalamu wa kuunda mabomu. Alionekana kwenye picha ya kamera za usalama uwanja wa ndege akiwa pamoja na washukiwa wawili ambao inadaiwa walijilipua wakati uwanja wa ndege wa Zaventem. Alikuwa tayari anatafutwa na polisi kuhusiana na mashambulio ya Paris mwaka jana. Ripoti za kukamatwa kwake bado hazijathibitishwa na maafisa wa usalama. Taarifa za awali zilikuwa zimewatambua washukiwa walioonekana naye kwenye uwanja wa ndege kuwa ndugu wawili, Brahim na Khalid El Bakraoui. Watu 34 walifariki na zaidi ya 250 kujeruhiwa kwenye mashambulio mawili yaliyotokea katika uwanja huo wa ndege wa Zaventem na kituo cha treni cha Maelbeek. Kundi linalojiita Islamic State limedai kutekeleza mashambulio hayo. Bendera zinapepea nusu mlingoti nchini Ubelgiji. Taifa hilo limetangaza siku tatu za maombolezo ya kitaifa.

No comments:

Post a Comment